Kamanda wa polisi mkoa wa Singida, Celina Kaluba, akizungumza na waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) juu ya jeshi hilo kuzawadiwa mbwa.(Picha na Nathaniel Limu).
Na.Nathaniel Limu
Jeshi la Polisi Mkoani Singida linatarajia kuendesha mafunzo ya ulinzi kwa kutumia mbwa ili waweze kutumika katika shughuli za ulinzi shirikishi mkoani humo.
Hayo yamesemwa juzi jumamosi na Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Singida,Celina Kaluba, alipokuwa akipokea zawadi ya mbwa mmoja aina ya ‘Germany Sheephed’ kutoka kwa shirika la kutetea haki za Wanyama Tanzania (TAPO).
Amesema mbwa wakitumika vizuri wanaweza kusaidia kukabiliana na vitendo vya uhalifu.
Kaluba ameongeza kuwa ili kuimarisha ulinzi, kuanzia sasa jeshi lake litawaomba madaktari wa mifugo wanaopenda kutibu mbwa wawe wanaambatana na askari polisi wanaotoa mafunzo kwa mbwa.
Aidha amesema mbwa ni rafiki wa binadamu hata katika mataifa mengine duniani yalikuwa yakiwafanya kama kivutio, lakini hivi sasa wamebadilika na kuanza kuwatumia katika shughuli mbali mbali za ulinzi, kwa mfano kutambua maeneo yalipofichwa mabomu na dawa za kulevya.
Kamanda huyo amesema uamuzi wa kuwafuata majumbani watu wanaofuga mbwa ni wa kuwaondolea usumbufu wa kuitafuta huduma hiyo.
Ameongeza kuwa kutokana na wananchi kukubali kuliunga mkono jeshi la polisi katika suala zima la ulinzi shirikishi, Jeshi hilo litawatambua wananchi hao kama wadau.
Kamanda Kaluba alilishukuru shirika la TAPO na kusema kuwa limeonesha jinsi gani lilivyoguswa na tatizo la vitendo vya uhalifu nchini.
Kwa upande wake katibu mkuu wa TAPO Master George, amesema shirika lake limeamua kumzawadia kamanda huyo mbwa mwenye thamani ya shs. 200,000= ambaye ni bingwa katika masuala ya ulinzi ili kuunga mkono kazi kubwa ya kuimarisha ulinzi mkoani Singida.








