Picha mbalimbali za mahema yaliyochomwa moto na watu waliovamia kambi ya kampuni ya utafiti na uchimbaji madini ya Shanta iliyopo katika kijiji cha Sambaru wilayani Singida. (Picha na Nathaniel Limu).
Na Nathaniel Limu.
Jeshi la polisi mkoani Singida limeanzisha msako mkali kuwanasa wavamizi wote waliovamia kambi ya utafiti na uchimbaji madini ya Shanta, iliyopo katika kijiji cha Sambaru na kisha kufanya uharibifu mkubwa wa mali na uporaji.
Kamanda wa polisi mkoa wa Singida Celina Kaluba amesema wameshatuma askari wa kutosha kwa ajili ya kufanikisha shughuli hiyo na kupeleleza kiini cha uvamizi huo.
Amesema tayari wamekwisha nasa baadhi ya watuhumiwa wa uvamizi huo wakiwa na baadhi ya mali waliyopora kwenye kambi hiyo yenye wakazi zaidi ya 70.
“Kwa sasa siwezi kuwataja majina yao wavamizi hao ambao tumewakamata. Nitafanya hivyo mara tutakapomaliza shughuli yetu hapo Sambaru”,alisema.
Kwa upande wake mfanyakazi wa Shanta ambaye ameomba jina lake lisitajwe kwa madai kuwa sio msemaji wa kampuni hiyo, amesema wanamshukuru Mungu kutokana na tukio hilo kufanyika nyakati za mchana kwa kuwa lingefanyika usiku, watu wangeweza kupoteza maisha yao.
Amesema wavamizi hao ambao walikuwa wamebeba silaha za jadi, wamechoma moto na kuteketeza mahema 11 na mengine tisa wameyachana.











